Wednesday, February 26, 2014

MAKALA

TAIFA LINAVYOTAFUNWA NA MIGOGORO YA ARDHI

Ndugu Mhariri,
Najitokeza katika ukurasa wako huu nitoe yangu ya moyoni,hii ni kutokana na Taifa letu kuandamwa na migogoro ya Ardhi isiyokwisha.
Kwanza napenda kumpa pole,mzazi wa mtoto wa miaka 12 aliyefariki kwa kufyatuliwa risasi na aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi na Diwani wa Kata ya Kisesa Clement Mabina na pili nawapa pole Familia ya marehemu Clement Mabina,tatu nawapa pole viongozi wa Mkoa wa Mwanza kwa kuondokewa na raia ambao kwa namna moja kila mmoja alikuwa akitegemewa na familia yake na Taifa kwa mchango wake wa mawazo na mengine mengi.
Nikiwa nasoma shuleni mwalimu wangu wa kwanza kunifundisha somo la Siasa ambaye ni Boniventura Shebo Nkuba aliwahi kutufundisha kuwa ili Taifa lolote liweze kuendelea linahitaji vitu vine Ardhi, watu,Siasa safi na Uongozi bora.
Nilijisikia amani kusikia hivyo na nilijifunza kuwa kilichokuwa kikifundishwa endapo kingekuwa na ufuatiliwaji thabiti na wenye mamlaka huenda kingeweza kuwa ni dira ya Taifa kama ilivyokuwa wakati wa Azimio la Arusha.
Serikali ya Awamu ya kwanza hadi ya Nne tumeendelea kusikia kauli hiyo lakini sasa,ufuatiliaji na utimilifu wa dira hii unaenda ukipotea taratibu na watu wakiendelea kupoteza uvumilivu.
Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Jakaya Kikwete imekuwa ikipiga kelele kuhusu kuondolewa urasimu katika umiliki wa Ardhi kwa wananchi kwanza na baadaye kwa wawekezaji,katika sekta mbalimbali nchini,ikiwemo viwanda,biashara na kilimo.
Cha kushangaza, watendaji wa Serikali wameshindwa kuwajibika kwa wananchi walioiweka Serikali hiyo madarakani kuhusu kuwapatia Elimu juu ya sheria ya Ardhi, tumeendelea kushuhudia madhara makubwa yanayoendelea kulitafuna Taifa letu na watu wake.
Kila kukicha vilio,ugomvi kati ya wananchi wakulima na wafugaji,wawekezaji na wananchi na hatimaye tunashuhudia Vigogo  kujichukulia maeneno ya wananchi kwa kutoa fedha kidogo nazo zikiishia mikononi mwa wajanja wachache wanaoongoza serikali za vijiji au hakuna kabisa hata shilingi inayowasilishwa ili kuchangia maendeleo katika maeneo husika.
Tunaona mfano kwa aliyekuwa mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi na dunia wa Kata ya Kisesa jijini Mwanza marehemu Clement Mabina,kwa mujibu wa mtoa taarifa Mgogoro kati ya wananchi na kigogo huyo unaonyesha  kuwa haukuwa mpya, ulikuwa ni wa muda mrefu, tunaona jinsi wananchi wanavyoweza kuwa na uvumilivu na hatimaye uvumilivu ukiwashinda matokeo yake kuamua liwalo na liwe.
Kufuatia kushamiri kwa migogoro ya Ardhi hii Nchini ni dalili tosha kuwa iwapo serikali haitachukua hatua za haraka huenda hali ikawa mbaya zaidi.
Ninayo mifano mingi ya migogoro hiyo katika maeneo mbalimbali nchini,wilayani kishapu kuna maeneo yaliyochukuliwa na mwekezaji na wananchi mpaka leo wanalia na hakuna anaye wasikiliza kilio chao,Mpanda,Kibaha, Nyamongo, Karagwe,Ngorongoro na maeneo mbalimbali Mkoani Morogoro,Mbeya,Dodoma na maeneo mengine  ipo migogoro inayofukuta.
Ukisikiliza vyombo vya habari utasikia viongozi wakitoa ahadi lukuki kuhusu kulinda maslahi ya taifa na huku wakisisitiza kuwa suala la Ardhi ni nyeti na wananchi wapewe kipau mbele kwanza katika kumilikishwa Ardhi kabla ya wageni.
Ukifuatilia kwa undani vigogo walio wengi pamoja na matajiri wenye fedha zao wamejimilikisha maeneo makubwa huku wananchi wakiporwa maeneo na wakipiga kelele kila kukicha bila mafanikio.
Kwa mfano Wilayani Muleba kuna kigogo mmoja ambaye aliwahi kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera anayedaiwa kujipatia ardhi yenye ukubwa wa ekari 8000 zaidi ya hekari alizoziomba, ambapo kigogo huyo aliomba kupatiwa ekari 2000, uombaji ambao hata hivyo haukufuata kanuni na taratibu, ikiwemo ushirikishwaji wa wananchi haukuzingatiwa,hivyo kuzua mgogoro mkubwa.

Hivi kweli kwa hali hii tunaweza kukubaliana kuwa ili taifa liendelee tunahitaji Ardhi,watu,siasa safi na uongozi bora?
Tanzania imebarikiwa kuwa na Ardhi tena iliyosheheni Madini kama Almasi, dhahabu, Urani, gesi, mafuta, misitu,Wanyama, Mito, Maziwa, na Bahari,rasrimali zote hizi zikiwa ni mali yetu sote.
Enzi za utawala wa Kanal Muamar Ghadaff wa Libya Watanzania wote leo ,kila mmoja wetu angeingiziwa fedha  kwenye Akaunti yake ili aweze kunufaika na mali asili kutoka kwa Mungu lakini si kwa nchi kama Tanzania kwa watu waliojenga imani ya Mimi kwanza wengine baadaye kila mtu anavutia kwake.    
Nina ushahidi kuwa Serikali pamoja na raia wake wote hakuna mtu hata mmoja anayetozwa ushuru au kodi na mwenyezi Mungu kwa ajiri ya maliasili hizi,vitu hivi vimepatikana bure kabisa.
Iweje leo tuhangaike Matibabu?
Iweje leo tuhangaike Ada za watoto wetu?
Iweje leo tuhangaike Madawa na majengo ya zahanati  na hospitali?
Iweje leo kina mama wajawazito wajifungue kwa kununua gloves na dawa za kuzuia damu wakati wa uzazi?
Je wapo viongozi tulio nao ni bora na wanaosimamia sera na mipango ya serikali ili kuendeleza wananchi wake katika sekta za kilimo, Afya na nyinginezo?
Je siasa zinazofanywa na wanasiasa wetu ni siasa safi kama nilivyoanza kusema hapo awali?
Tunashuhudia viongozi wa ngazi za chini leo wanavyoifuga migogoro hii kwa manufaa yao na kupelekea wananchi kujichukulia sheria mkononi,Mkoani Morogoro na huko Ngorongoro wananchi wamjichukulia sheria mkononi huku wakivamia vituo vya polisi kwa lengo la kuwakomboa wenzao na matokeo yake hali hiyo ikapelekea mauaji ya raia kwa risasi za moto je hali hii ikiendelea kwa mfumo wa kisiasa Taifa letu litakuwa mahali salama pa kukimbilia?.
Angalia wawekezaji wa migodi inayomilikiwa na kampuni ya  Barrick kule Buzwagi  jinsi walivyochukua maeneo huko Mwendakulima na kuwaweka wananchi katika hali ngumu huku wakivuta vumbi lenye kemikali na huku wakipiga kelele zao kwa viongozi bila mafanikio!
Hivi kweli iwapo wananchi watakapoingiwa na shetani wa kukosa uvumilivu kama ilivyotokea kwa marehemu Clement Mabina Nchi yetu bado itakuwa ni sehemu salama ya kuishi na kisiwa cha amani kama inavyojulikana katika jumuia ya kimataifa!
Rai yangu kwa viongozi wa serikali pamoja na wananchi hebu tuombe ibilisi huyo apishe mbali viongozi wa serikali nao watoe kipaumbele katika kutoa Elimu ya uraia pamoja na sheria ya Ardhi kwa kushirikiana na makundi mbalimbali zikiwemo asasi za kiraia ili kulinusuru taifa letu kuingia katika migogoro mikubwa kati ya raia na Serikali,matajiri na maskini.
Mungu ibariki Tanzania!
Mwandishi wa makala hii ni mwanaharakati wa Haki za Binadamu
0785 118118

0 comments:

Post a Comment