Friday, January 30, 2015




Waliopigwa risasi na Askari wa Mgodi wailalamikia Serikali.
Na Antony Sollo, Kishapu.

 WANANCHI wa kijiji cha Maganzo na vitongoji vyake wameilalamikia Serikali kwa kushindwa kusikiliza kero na adha wanayoipata kutoka kwa Mwekezaji wa mgodi wa WDL kufuatia mashambulizi ya mara kwa mara yanayofanywa na Askari wa Mgodi huo

Jilala Miligwa ameliambia Tanzania Daima kuwa amechukua hatua ya kufikisha kilio hicho kwa Rais Jakaya Kikwete akimuomba aingilie kati suala hili baada ya yeye na wenzake tisa kujeruhiwa mgodini hapo huku kukiwa hakuna juhudi zozote zinazofanyika ili waweze kulipwa fidia kutokana kushambuliwa kwa risasi za moto na askari wa mgodi huo.
Akizungumza kwa niaba ya wenzake wanane Jilala alisema kuwa ameamua kupeleka malalamiko hayo kwa Rais Kikwete kutokana na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Sospeter Muhongo kushindwa kulitafutia ufumbuzi suala hilo akiwa katika ziara yake Jan 8 Mkoani Shinyanga.
 Katika ziara hiyo Muhongo alipokuwa akiongozana na Mbunge wa Jimbo la Kishapu Suleman Nchambi na kupatiwa taarifa za kujeruhiwa kwa vijana hao aliahidi kutatua tatizo lao mapema kwa kuuagiza uongozi wa mgodi kuwalipa fidia.
 “Ndugu zangu naomba niwahakikishie,Serikali yenu iko tayari kuwasikiliza na kutatua matatizo yenu hivyo kuanzia sasa naagiza uongozi wa Mgodi wa Mwadui uwalipe fidia haraka iwezekanavyo” alisema Muhongo.

Jilala ameliambia Tanzania Daima kuwa Muhongo pamoja na Mbunge waliwaahidi vijana hao kuwa wangekutana na Uongozi wa Mgodi januari 19 mwaka huu lakini cha kushangaza si Mbunge wala Waziri aliyefika kwa lengo la kutekeleza ahadi hiyo.

Jilala alilalamikia tabia ya Mbunge huyo kutoa ahadi ambazo mara kadhaa hazitekelezeki na anapoulizwa anajibu kisiasa jambo ambalo linawakera wananchi hao.

“Nchambi amekuwa na tabia ya kutumia matatizo yetu kujizolea umaarufu ndani ya Bunge na kwenye majukwaa ya siasa akitumia maneno matamu ambayo yanafanana na ukweli lakini utekelezaji wake ni hovyo…alisema Miligwa.

“Mbunge wetu amekuwa akituahidi kuwa atatusaidia kupata fidia bila mafanikio,tumeona kuwa anapenda kujipendekeza kwa viongozi wa kitaifa pindi wanapokuwa na ziara Mkoani hapa.

 Akichangia katika vikao vya Bunge Nchambi amekuwa hodari wa kutoa kauli na kujigamba kuwa yupo tayari kufa kwa ajili ya wanyonge ambao wanapoteza haki zao lakini anachokisema  ni tofauti na anachokitenda” alisema Miligwa.

Kabla ya kujiuzuru Tanzania Daima lilimtafuta aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini,Sospeter Muhongo ili aweze kutoa ufafanuzi wa malalamiko hayo lakini hakuweza kupokea simu kwa wakati.

 Baada ya kusumbuliwa kwa kuandikiwa ujumbe mfupi wa simu ya mkononi ndipo alipofunguka na kuweza kujibu japo hakuweza kutoa ufafanuzi juu ya ufumbuzi wa vijana hao kupitia Wizara Nishati.

Ujumbe mfupi wa Waziri ulikuwa hivi” 
“Huo ni uzushi! Mimi niliagiza uchunguzi ufanyike wa wale wote wanaolalamika! Utalipa bila kuchunguza?utalipa bila kufuata sheria na kanuni zake?” kwa nini vijana hawa wanaogopa kwenda Mahakamani kwenye haki? Kwa nini hawafungui kesi Mahakamani? Waende Mahakamani “alihoji Prof Muhongo.

Tanzania Daima lilipotaka kujua ni hatua gani zitafuata baada ya uchunguzi huo kukamilika ,Waziri Muhongo alisema kuwa ni vyema kuwa waangalifu,kama kweli unaonewa au umedhulumiwa hakuna sababu ya kusita kwenda Mahakamani Wizara itasaidia lakini kila upande unayo haki ya kwenda Mahakamani.

 Kuhusu ahadi ya Serikali kuwasaidia vijana hao Muhongo alisema kuwa baada ya uchunguzi huo atahakikisha Haki inatendeka pande zote zinazohusika,kama hawatakubaliana na kikao kitakachosimamiwa na Wizara basi itabidi waende Mahakamani.

“ili uweze kuupata ukweli ni lazima usikilize pande zote mbili,uamzi hauwezi kutolewa kwa kusikiliza upande mmoja” alisisitiza Muhongo. 

 Mbunge wa Jimbo la Kishapu alipopigiwa simu 0767 444 148 ili kutolea ufafanuzi juu ya malalamiko ya wananachi hao alikata  simu na hata alipopelekewa ujumbe akiombwa kutolea ufafanuzi juu ya malalamiko hayo alijibu kwa meseji fupi “Siyajui”

Mwisho.

0 comments:

Post a Comment