Tuesday, August 5, 2014

Mfanyakazi wa Mzani wa Usagara ahojiwa na Takukuru kwa saa saba

Mfanyakazi wa Mzani wa Usagara ahojiwa na Takukuru kwa saa saba 
 Ni kwa tuhuma za kuomba na kupokea Rushwa
Na Antony Sollo Mwanza.
August 5.2014.

MFANYAKAZI wa Mzani wa Usagara Jijini Mwanza,Yusuf Kasumula amehojiwa kwa zaidi ya saa saba na Maafisa wa Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU,akituhumiwa kuomba na kupokea Rushwa akiwa kazini imefahamika.


Tukio hilo lilitokea August 2 mwaka huu majira ya saa 4 : 00 Asubuhi katika eneo la Usagara Mzani wa Usagara baada ya Photidas Kennedy ( 40 ) Dereva wa gari namba za usajili T 864 CGD aina ya Fusso lililokamatwa usiku wa terehe 02 August 2014 saa 4:00 usiku na kuombwa Rushwa ya shilingi laki moja,akidaiwa kuzidisha uzito wa mzigo katika gari lake.

Imedaiwa kuwa mtumishi wa Mzani wa Usagara Yusuf Kasumula aliomba kiasi hicho cha fedha ili amuachilie Kennedy aendelee na safari yake jambo ambalo Kennedy alilipinga vikali.

Baada ya kusumbuliwa muda mrefu Kennedy alilazimika kutoa kiasi hicho cha fedha shilingi 75,000  na kumpa Kasumula na baada ya hapo Kennedy aliomba msaada kwa Maofisa wa Takukuru. 

Tukio hilo liliripotiwa kwa mwandishi wa habari wa gazeti hili ambaye alishirikiana na Kennedy kutafuta ufumbuzi wa tukio hilo ambapo kwa pamoja walitoa taarifa kwa Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza Christopher Cyprian Foime  ambaye aliwasiliana na Uongozi wa Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa Mkoa wa Mwanza.

Kamanda wa Takukuru Mkoa Mwanza aliwajulisha Maafisa wa Taasisi hiyo Wilaya ya Misungwi Julian Augustine wakiwa na Dereva Bahati Nzumbi walifika Usagara na kufanya mahojiano na Yusuf Kasumula. 

Wakizungumza na Tanzania Daima baadhi ya Madereva wanaotumia Mzani huo kutoka Mikoa mbalimbali nchini ,wamelalamikia kitendo cha kupima katika Mizani ya Mikoa mingine na Uzito wa Mizigo yao kuwa sahihi,lakini wanapofika katika Mzani huo uzito wa Mizigo yao hubadilika na matokeo yake kuombwa rushwa na wakikataa kutoa rushwa hupigwa faini kwa lengo la kukomolewa.

Madereva waliopatwa na mkasa huo ni Khasim Hausi dereva wa Lori lenye namba za Usajili T 210 CAQ aina ya Fusso.

 Khasimu ameliambia Tanzania Daima kuwa wakati anatoka Karagwe na kupima Mzani wa Kyaka mzigo wake ulikuwa na Kilo 6000 mbele na upande wa nyuma ilikuwa ni kilo 9800.
Khasim amedai kuwa alipofika Mzani wa Usagara Mzigo wake ulipimwa na kuonyesha kuwa ulikuwa umezidi kilo 250 jambo ambalo hakukubaliana nalo maana hakuongeza mzigo wa aina yoyote njiani.

Baadaye Khasim aliombwa atoe fedha kiasi ambacho ni kikubwa na akalalamikia unyanyasaji wanaofanyiwa Madereva wanaotoka Mikoa mbalimbali nchini na watendaji wa Wakala wa Barabara TANROADS Mkoa wa Mwanza. 

Baada ya kufuatwa na waandishi wa habari na kuhojiwa kuhusiana na madai ya Khasim na Kennedy Kasumula alikiri kuwafahamu Madereva hao na kusema kuwa Magari yao yalizidisha uzito.
Kuhusu kulipa faini na kushindwa kupewa risiti Kasumula alisema kuwa “taratibu za Ofisi ya TANROADS unalipa kwanza na risiti utapewa baada ya mzigo wako kukaa vizuri.”
Katika kile kinachodaiwa kuwatisha Maafisa wa Takukuru,mzani wa Usagara unasoma nyaraka zake tofauti na sehemu zingine kwa kuwa iwapo utapima mzigo wako hapo tarehe 5 August mwaka huu nyaraka zako zitaonyesha ulipima tarehe 6 August jambo ambalo madereva na wadau mbalimbali wamedai kuwa iwapo kuna makosa katika usomaji wa tarehe basi kuna mashaka makubwa hata katika upimaji wa uzito wa mizigo.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima umebaini kuwa,kuna dalili za wizi na ubadhilifu mkubwa unaofanyika katika Mzani wa Usagara kwani hata usomaji wa nyaraka katika mzani huo hauendani na uhalisia.

Akizungumzia utata wa kusoma tarehe ya siku inayofuata badala ya tarehe husika Mhandisi wa Tanroads Mkoa wa Mwanza Pius Joseph aliliambia Tanzania Daima kuwa ni kweli kuna tatizo la usomaji wa tarehe katika mzani huo.
“Ni kweli kuna tatizo la kusoma kwa tarehe katika mzani huo tunalifahamu ni la muda mrefu,tutalishughulikia.”alisema Joseph.
Kukiri kwa Mhandisi huyo juu ya utata katika kusoma kwa tarehe kumethibitisha madai ya kuchakachuliwa kwa Mzani wa Usagara.
Wakizungumzia kwa uchungu dhidi ya uonevu wanaofanyiwa na watendaji wa Mzani wa Usagara Madereva mbalimbali wanaotumia Mzani wa Usagara wameiomba Serikali ishughulikie tatizo hilo kabla hawajatangaza mgogoro mkubwa ambapo walisema ifikapo Augosti 15 wataanza mgomo utakaoendeshwa bila kikomo kwa kuweka magari kuzuia huduma ya Usafiri wa aina yoyote kwa barabara ya Usagara Misungwi ,Kigongoferry na Sengerema.
 Maafisa hao wa Takukuru walichukua takribani masaa saba kuchukua maelezo ya   na Yusuf  na baada ya mahojiano hayo,waliondoka na nyaraka mbalimbali zinazotumika katika Mzani uo kwa uchunguzi.  
Mwisho.





























0 comments:

Post a Comment